"HAKIELIMU" SHULE ZA KATA KUPATA UMEME

SERIKALI imesema itakamilisha ujenzi wa shule za Sekondari 1,200 kwa kuweka miundombinu muhimu ikiwemo umeme kupitia Mpango wa Maendeleo wa Elimu ya Sekondari awamu ya pili.
Kauli hiyo imetolewa leo Bungeni mjini Dodoma na Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa, Mhe. Majaliwa Kassim Majaliwa wakati akijibu swali la Mbunge wa Dodoma Mjini, Mhe. Dk. David  Mallole, aliyetaka kujua Serikali ina mpango gani wa kupeleka umeme kwenye Shule za Kata hasa za Bweni.
Mhe.Majaliwa amesema kuwa kwa awamu ya kwanza Serikali imeanza kukamilisha ujenzi kwa shule 264 kwa thamani ya shilingi Bilioni 56.3 ambapo suala la umeme wa gridi ya taifa na  umeme wa jua limepewa kipaumbele.
Ameongeza kuwa Serikali kupitia mfuko wa wakala wa usambazaji umeme Vijijini (REA) imedhamiria kusambaza umeme katika zahanati, shule na visima vya maji vilivyo katika maeneo yatakayonufaika na huduma hii ya umeme Vijijini.
“Mpaka sasa, Serikali imewezesha shule za sekondari 3,385 sawa na asilimia 75 ya shule zote za sekondari nchini kuwa na huduma ya umeme” amesema Mhe. Majaliwa.
Ameongeza kuwa Serikali itaendelea kishirikiana na wadau na kupitia miradi mbalimbali ya maendeleo kuhakikisha dhamira ya kuziwezesha shule na maeneo mengine yanayotoa huduma za jamii yanakuwa na huduma ya uhakika ya umeme.


EmoticonEmoticon