SERIKALI KUUNDA TUME YA KITAALAMU YA KUFANYA MAPITIO MAKUBWA YA MFUMO WA

Mfumo wetu wa elimu kwa muda mrefu umeonesha udhaifu katika usimamizi, uendeshaji, udhibiti na ugharimiaji tangu Taifa letu lilipo amua kufanya ugatuzi wa madaraka, uliopelekea sekta ya elimu kuendeshwa chini ya wizara tatu tofauti.
Ili kufanya mabadiliko katika Elimu, Tuungane kuitaka serikali kuunda tume ya kitaalamu ya kufanya mapitio makubwa ya mfumo mzima wa elimu inayotolewa tanzania bara ili kwenda sambamba na kasi kubwa ya mabadiliko ya kiuchumi duniani.
KWA KUWA, Elimu mpaka Kidato cha nne hutolewa bure lakini elimu bora inauzwa.
NA KWA KUWA, imebainika kwa Tanzania ina mfumo wa elimu usiojali usawa kwa kiwango cha juu, mfumo kwa ajili ya makundi mawili, kundi moja la matajiri, na kundi lingine la masikini, na mfumo wa elimu ya shule bora za umma kwa ajili ya watu wa kada ya katikati
NA KWA KUWA, Asilimia 16 pekee ya bajeti ya sekta ya elimu hutengwa kwa ajili ya kugharimia Maendeleo ya sekta ya elimu wakati jumla ya Taasisi na Wakala 88 ambazo zinatafuna asilimia 84% ya bajeti nzima ya Sekta ya Elimu (bilioni 3,887)
NA KWA KUWA, Mfumo wa elimu hapa nchini unaundwa na kusimamiwa na wizara tatu tofauti ambapo wizara ya elimu pekee kuna zaidi ya taasisi na wakala 88 zilizo chini ya wizara hii ya Elimu, Sayansi Teknolojia na Ufundi, ambazo bajeti yake ya matumizi ya kawaida yanamaliza fedha zote hata kabla hazijaanza kuleta Maendeleo.
NA KWA KUWA, Ukaguzi wa Shule za Msingi na Sekondari nchini hazikaguliwi kwa kiwango cha kuridhisha ambapo asilimia 9.1 ya shule za msingi nchi nzima na asilimia 21.4 ya shule za sekondari zote nchini ndizo hukaguliwa kwa mwaka kutokaka na ugharimiaji hafifu.
NA KWA KUWA, Ugharimiaji hafifu wa sekta ya elimu nchini umedumaza kiwango cha watoto kujifunza darasani kwa zaidi ya miongo miwili iliyopita ambapo tafiti zinaonesha kuwa “uwezo wa watoto kujifunza kusoma na kuhesabu ni mdogo sana Tanzania” inakadiriwa kuwa asilimia 45% pekee ya watoto wa darasa la 3 wanaweza kusoma kwa ufasaha hadithi ya Kiswahili ya darasa la 2, wakati asilimia 19 pekee ya watoto hao hao wa darasa la 3 wanaweza kusoma kwa ufasaha hadithi ya kingereza ya darasa la 2.
NA KWA KUWA, Kuna pengo kubwa kati ya masikini na matajiri katika mfumo wa elimu ambapo inakadiriwa kuwa watoto 3 kati ya 10 wenye umri kati ya miaka 13 wanatokea katika familia masikini sana (ultra-poor households) ndio walifaulu zoezi la kusoma hadithi za kingereza na kiswahili.
NA KWA KUWA, Utekelezaji wa Sera ya Elimu bure una uwezekano mkubwa wa kuongeza maafa katika ubora wa elimu chini kwa sababu Sera hii imeongeza idadi kubwa ya wanafunzi wanaodahiliwa katika shule za msingi na shule za Sekondari katika shule za umma bila kuwa na ongezeko la bajeti ya uendeshaji, usimamizi na ugharimiaji wake pamoja na kuwa na muunganiko kati ya elimu ya kati na elimu ya chini na elimu ya juu.
NA KWA KUWA, Watoto waishio familia masikini vijijini ndio huathirika zaidi na usimamizi, uendeshaji na ugharimiaji duni wa elimu nchini, ambapo watoto 4 kati ya 10 waliopewa zoezi la kusoma na kuhesabu vijijini ndio waliofaulu, hii maana yake ni kuwa watoto 6 kati ya 10 kutoka vijijini uwezo wao wa kusoma na kuhesabu upo duni sana, ukilinganisha na watoto wa mijini ambao wao 6 kati ya 10 walifaulu zoezi la kusoma na kuandika.
NA KWA KUWA, Mazingira ya watoto kujifunza bado yapo duni sana kutokana na ugharimiaji hafifu, ambapo Utafiti wa Twaweza ulibaini kuwa asilimia 44 pekee ya shule za umma ndizo zinatoa huduma ya chakula shuleni, wakati asilimia 46 pekee ya shule za umma ndizo zina maji safi ya kunywa, na asilimia 31 ya shule zote za umma ndizo zina maktaba wakati kitaifa wanafunzi 30 wanatumia kitabu kimoja kujifunzia.
NA KWA KUWA, Imebainika kuwa Mpango wa Maendeleo wa Miaka 5 katika elimu umepoteza mwelekeo kuhusu ugharimiaji wa sekta ya elimu, ambapo kuna upungufu mkubwa wa ugharimiaji wa elimu ndani ya kipindi cha miaka 5 ijayo, ambapo Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa miaka 5, unapendekeza ugharimiaji wa elimu ya misingi uwe Shilingi Bilioni 1,357 ambazo ni sawa na asilimia 28% ya fedha zote zinazotarajiwa kutengwa kwa miaka yote mitano (Bilioni 4,898.92.)
NA KWA KUWA, Elimu ya Msinig imetengewa bajeti finyu ya Maendeleo kwa mwaka wa fedha 2016/17 ambapo Shilingi Bilioni 156.73 zimetengwa kwa ajili ya Maendeleo ya elimu ya Msingi ambazo ni sawa na asilimia 17% ya fedha zote zilizotengwa kwa ajili ya bajeti ya Maendeleo ya wizara Elimu, Sanyansi, Teknolojia na Ufundi katika mwaka wa fedha 2016/17.
NA KWA KUWA, Mpango wa Maendeleo ya “elimu bure” katika shule za Sekondari umetengewa asilimia 4% pekee ya fedha zote katika miaka mitano ijayo, ambapo hakuna uhalisia katika ugharimiaji wa mpango wa elimu bure nchini kwa shule za sekondari.
NA KWA KUWA, Waalimu wamekuwa na malalamiko ya muda mrefu ya madai ya stahiki zao yenye jumla ya shilinigi bilioni 408 na zaidi, wakati motisha na ari yao ikizidi kushuka siku hadi siku.
Kwahiyo basi tuungane kwa pamoja KUSAINI NA KUSHARE ili kwamba serikali ituundie tume ya kitaalamu ya kufanya mapitio makubwa ya mfumo wa elimu inayotolewa tanzania bara ili kwenda sambamba na kasi kubwa ya mabadiliko ya kiuchumi duniani.


Mhe. Mbashe amwomba Rais Magufuli kufanya marekebisho mazingira ya uendeshwaji Biashara


Napenda kuchukua fursa hii kwa heshima kubwa kabisa na kwa niaba ya wananchi wenzangu wa Jimbo la Nzenga Mjini kumpongeza Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Joseph Pombe Magufuli kwa uamuzi aliouchukua wa kuivunja Bodi ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na kumfuta kazi mwenyekiti wa Bodi hiyo Bw. Bernard Mchomvu, kwa kutofuata maagizo ya Mhe. Rais na matakwa ya Sheria ya Benki Kuu ya Tanzania ya mwaka 2006, kifungu cha 31 na 32 ambavyo vinaelekeza Mashirika ya Umma na Taasisi za Serikali kuweka fedha zao katika akaunti maalumu zilizopo Benki Kuu.
Uamuzi huo sio tu unawanufaisha walipa kodi wa Taifa letu lakini pia unakomesha tabia za matumizi mabaya ya madaraka na fedha za umma kwa kujitajirisha na kujinufaisha isivyo halali kwa baadhi ya Watendaji Wakuu wa Mashirika ya Umma.
Namshauri Mhe. Rais kufanya marekebisho makubwa katika mfumo mzima wa uanzishaji, uendeshaji na uratibu wa biashara nchini ili kuongeza ajira nchini, kwa kuwa ripoti ya Benki ya Dunia (2016) ya kufanya biashara Tanzania (Doing Business Tanzania- 2016) inaonesha Tanzania kutofanya vizuri katika Sera na Sheria za usajili wa biashara mpya na mazingira ya uendeshaji wa biashara kuwa kushika nafasi ya 129 kati ya nchi 189. Kwa mujibu wa ripoti hiyo mjasiriamali akitaka kuanza biashara rasmi lazima avuke vihunzi 9 ndani ya takribani siku 26 ili aweze kufungua biashara yake! Vihunzi hivyo vinavunja moyo na kupunguza kasi ya ongezeko la ajira binafsi kwa njia ya ujasiriamali na pia inalipa Taifa hasara kwa kutokusanya kodi kutoka kwenye biashara hizi mpya kwa haraka na kwa wakati kutokana na urasimu uliopo.
Pamoja na hayo pia, namshauri Mhe. Rais, agize wizara ya wiwanda na biashara na wizara ya fedha kurekebisha sheria za kodi na biashara ili kuwezesha wepesi, urahisi na uharaka wa kukusanya kodi na kuwezesha wafanyabiashara wadogo kufanya biashara kwa uhuru. Ripoti ya Doing Business Tanzania, (2016) imebainisha kuwa makampuni yanayolipa kodi huchukua saa 179 kujaza fomu za marejesho hivyo kuifanya Tanzania kuwa na utaratibu mgumu wa kulipa kodi na kushika nafasi ya 150 kati ya nchi 189 duniani kwa ugumu wa taratibu za kulipa kodi. Tukiondoa ugumu huo na kuweka wepesi, kasi ya kukusanya mapato ya kodi itaongezeka na mapato pia yataongezeka! Kwa umahususi Serikali inaweza kuanzisha kituo kimoja cha biashara kwa wafanyabiashara wadogo (one stop business center) kitakachotoa motisha kwa kuratibu uanzishaji wa biashara husika mpaka kulipa kodi kwa njia za digitali na mifumo ya TEHAMA. Vituo hivi viwepo kuanzia ngazi ya Serikali za Mitaa ili kurahisisha shughuli za uanzishaji wa Biashara na uwekezaji kutokea chini.
Marekebisho hayo ya sheria za kodi na biashara yalenge zaidi kutengeneza ‘Business Incubation’ na Misamaha ya kodi (Tax holidays) kwa wafanyabiashara wadogo wanaoanza biashara ili kusaidia kukuza biashara kuliko hali ilivyo hivi sasa ambapo biashara ndogo zinakabiliwa na mzigo mkubwa wa kodi na Tozo za ushuru mbalimbali katika halmashauri zetu kwa mfano Leseni, kodi ya huduma, kodi ya mapato, na kodi za majengo.
Pia kama taifa umewadia wakati Mhe. Rais awaagize BoT na Wizara ya Fedha katika kipindi cha miaka hii mitano ya awali kubadili ‘Modeli ya Uchumi’ wetu kutoka ‘Consumption module’ kwenda kwenye ‘Investment module’ na hii iendane na mabadiliko makubwa ya ‘Tax structure’ yetu na sheria za Uwekezaji na Biashara na kutengeneza motisha (Incentive package) za kisekta na si motisha za ya mwekezaji mmoja mmoja. Sekta muhimu ambazo zinahitaji kupewa kipaumbele kwenye hiyo new module ni sekta ya ngozi, na viwanda vya mazao ya kilimo.
Mwisho kabisa napenda kumhakikisha Mhe. Rais kuwa mimi binafsi kama mbunge, wananchi wa Jimbo la Nzega na Watanzania wengine wote tunaoamini katika uadilifu katika ofisi za umma, tunaendelea kumuombea ulinzi kwa Mungu, na tupo nyuma yake kumuunga mkono dhidi ya vita hii ngumu ya kupambana na ‘wapiga dili’ walioligeuza Taifa letu miaka 10 iliyopita kuwa shamba la bibi!

Asilimia 60 ya wananchi wanatamani kuamisha watoto wa kutoka shule za serikali



Asilimia 50 ya wananchi waliohojiwa katika utafiti wa kubainisha ubora wa elimu katika shule za serikali tangu kuanzishwa kwa mpango wa elimu bila malipo ya adda wamekiri elimu kuboreshwa licha ya kuwa asilimia 60 ya wananchi kutamani kuwasomesha watoto wao katika shule binafsi.

Utafiti huo pia umebainisha kuwa asilimia 34 ya wananchi wamelalamikia ukosefu wa waalimu, asilimia 30 wamelalamikia ukosefu wa madawati na asilimia 13 wakilalamikia ukosefu wa  madarasa, wengine wakilalamikia ufundishaji na ukosefu wa chakula kwa wanafunzi.

Mkurugezni mtendaji wa TWAWEZA Aidan Eyakuze amesema idadi hiyo ni ya wananchi kati ya 1,806 waliohojiwa Tanzania bara ambapo amesema asilimia 35 wamesema ubora wa elimu umemebaki palepale na wengine asilimia 15 wamesema ubora umeshuka kabisa.

Adha Tafiti hiyo pia imebaini kua asilimia 85 ya wazazi hawajiusishi na masuala ya masomo ya watoto wao, huku asilimia 83 imekuwa ni changamoto za miundombinu na matokeo mabaya ya wanafunzi na utovu wa nidhamu kwa wanafunzi


Utafiti huo umefanyika kati ya Agosti 7 na 14 mwaka huu hata hivyo baadhi ya wasomi walioshiriki uwasilishwaji wa ripoti hiyo kutoka chuo kikuu cha elimu wamesema matokeo hayo ayaendani na uhalisia wa hali ya elimu nchini na kwamba elimu aiwezi kuwanaubora kwa kipindi cha mwaka mmoja pekee.

Muswada wa Sheria ya huduma ya msaada wa kisheria kujadiliwa


Waziri wa Katiba na Sheria, Dkt. Harrison Mwakyembe amewataka wadau wa masuala ya sheria na wananchi kwa ujumla kutoa maoni yao juu ya muswada wa sheria ya kusimamia na kuratibu utoaji wa huduma ya msaada wa kisheria na kutambua wasaidizi wa kisheria, muswada ambao umesomwa kwa mara ya kwanza bungeni.

Akiongea na waandishi wa habari leo Jijini Dar es Salaam Dkt. Harrison Mwakyembe amesema muswada huo unalenga kusaidia zaidi wananchi wasiojua sheria, na wasio na uwezo wa kuwalipa wanasheria jambo ambalo litatimiza azma ya serikali ya watu wote kuwa sawa mbele ya sheria na kupata haki bila ubaguzi.

Dkt. Mwakyembe amesema ni vyema wasaidizi zaidi ya 80 ambao bado awajapewa mafunzo na kusajiliwa na wizara yake kufuata taratibu zilizowekwa na wizara yake kwani serikali bado inatambua msaada wao katika kuhakikisha kuwa wananchi wanaelimishwa kuhusu haki zao.

Naye Mratibu wa Sekretarieti ya msaada wa kisheria kutoka wizara ya Katiba na Sheria Bw. Daniel Lema amesema mara baada ya sheria hiyo kuanza kazi wananchi wataweza kupata wasaidizi wa kisheria katika maeneo yao kwani wizara hiyo itakuwa na uratibu mzuri wa kufanya kazi na mashirika ya sheria na wasaidia wa sheria.

Mama Samia: Mikakati ya kuhakikisha wanawake wanashiriki kikamilifu katika ngazi ya maamuzi utafikiwa. Makamu wa Rais Mhe. Samia Suluhu




Makamu wa Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan ameonyesha kufurahishwa na hatua zinazochukuliwa na baadhi ya nchi za Afrika katika kulinda na kutetea haki za binadamu hasa haki za wanawake na kusema kuwa bado kuna umuhimu mkubwa kwa nchi ambazo zinazosuasua kutekeleza mikataba hiyo kufanya hivyo ili kuhakikisha wanawake na watoto wanapata haki sawa katika jami.

Katika hatua nyingine, Makamu wa Rais amesema kuwa, Serikali ya Tanzania imepiga hatua kubwa katika kuwaajiri na kuwaingiza wanawake katika ngazi za maamuzi na kwa sasa mpango kabambe unafanyiwa kazi ili kuhakikisha sekta binafsi ambayo bado inaidadi ndogo ya wanawake kwenye ngazi za maamuzi kufanya hivyo.

Aidha amesema kuwa, tafiti mbalimbali zilizofanyika nchini zinaonyesha kuwa wanawake wengi walioingizwa kwenye bodi mbalimbali tayari bodi hizo zimeongeza ufanisi wa kazi maradufu.

Kwa upande wake, Rais wa Mahakama ya Afrika ya Watu na Haki za Binadamu Justice Sylvain Ore amesema kuwa mkutano huo ni muhimu kwani unalenga kujadili na kuweka mikakati inayolenga kuhakikisha nchi za Afrika zinazingatia na kulinda haki za bindamu hasa haki za wanawake kwa kiwango kikubwa.

Mkutano huo wa Mahakama ya Afrika ya Watu na Haki za Binadamu ambao unafanyika Jijini Arusha umehudhuriwa na wajumbe kutoka mataifa mbalimbali ya Afrika wakiwemo wajumbe kutoka Umoja wa Afrika AU na lengo la mkutano huo ni kutajadili masuala ya demokrasia na haki za binadamu katika nchi za Afrika.


Mufti Mkuu awataka waislamu kuchangia Damu siku ya Maulid


Mufti Mkuu wa Tanzania Sheikh Abubakar Zubeir Bin Ally ametangaza siku kuu ya kuzaliwa Mtume Muhamad ya Maulid maarufu kwa jina la Maulid Day, kitaifa itasomwa siku usiku wa tarehe 11 mwezi wa 12 mwaka 2016 katika Mkoa wa Singida Wilaya ya Iramba.

Akiongea na vyombo vya habari jijini Dar es salaam, Mufti Mkuu Sheikh Abubakar Zubeir amesema Maulid ya mwaka huu yataadhimishwa kwa namna tofauti ambapo waumini wa kiislamu kote nchini watatakiwa kuchangia damu na kufanya zoezi la usafi katika maeneo yao mara tu baada ya ibada.

Kipenzi chetu Bwana Mtume Muhammad amesema “Uislamu ni Usafi basi jisafisheni kwani hakika hataingia peponi isipokuwa Msafi, mwamisingi hii mimi mwenyewe nitaongoza usafi kufurahia kuendana na kuiga na kutekeleza mafundisho yake” amesema.

Aidha, amewataka viongozi wa Baraza kusimamia na kuhimiza amani ya nchi yetu na kutokuwa tayari kuwavumilia wale wote ambao wanataka kuharibu amani na utulivu katika nchi yetu.


Kauli mbiu ya Maulid ya mwaka huu ni Muislamu jitambue badilika amani na usalama ndio maisha yetu” hivyo nijukumu la kila muumini wa dini ya kiislamu na waumini wa madheebu mengine kutunza amani. Amesema.

Dkt. John Pombe Magufuli, leo amemuapisha Kamishna wa Polisi Diwani Athuman Msuya kuwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Kagera.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli, leo amemuapisha Kamishna wa Polisi Diwani Athuman Msuya kuwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Kagera.

Hafla ya kuapishwa kwa Kamishna Diwani Athuman Msuya imefanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wakiwemo Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Mohamed Chande Othman, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Mhe. George Boniface Simbachawene,  Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. George Mcheche Masaju, Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP) Ernest Mangu na Makamishna wa Polisi.

Baada ya kuapishwa kuwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Kagera, Kamishna wa Polisi Diwani Athuman Msuya amekula kiapo cha uadilifu kwa viongozi wa umma kilichoongozwa na Katibu wa Sekretarieti ya Maadili, Idara ya Viongozi wa Siasa Bw. Waziri Yahaya Kipacha.


Kamishna wa Polisi Diwani Athuman Msuya anachukua nafasi iliyoachwa wazi na Bw. Amantius Msole ambaye uteuzi wake ulitenguliwa. 

Wabunge wanaomiliki Mabasi ya Abiria waofiwa kuhujumu Muswada wa sheria za usafirishaji


Chama Cha kutetea  Abiria Nchini  Tanzania CHAKUA  kimemuomba Raisi Dr.John Magufuli na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ,kuzuia wabunge wanaomiliki mabasi ya kusafirisha abiria kutoshiriki katika kujadili Muswada wa sheria za usafirishaji  kwa madai kuwa wanamaslahi yao binafsi hivyo watashiriki kukwamisha muswada huo.
Wito huo umetolewa leo na Mwenyekiti  Taifa wa CHAKUA, Bw.Hassani  Mchanjama,wakati akizungumza na wanahabari,ambapo pamoja na mambo mengine amesema kuwa wamiliki wa Mabasi ya kusafirisha abiria wakiwemo wabunge, wamekuwa wakipitish sheria mbovu  kwa lengo la kujinufaisha wenyewe bila ya kujali haki za abiria.
"Kila mara Sumatra wanapopeleka muswada kuusu marekebisho ya sheria za usafirishaji Wabunge wenye mabasi wanaukwamisha, wakati kunasheria mbivu mbovu za sekta ya usafirishaji hawana huruma kabisa na wananchi wanavyoteseka zaidi wanaangalia maslahi yao" amesema
Ameendelea kufafanua kuwa baadhi ya wakatishaji tiketi wanapandisha bei ya nauli kinyume cha kiwango ambacho kimewekwa na Mamlaka ya Udhibiti wa Vyombo vya usafiri vya majini na nchi kavu(SUMATRA),ambapo ametolea mfano nauli za maeneo mengine hutozwa shilingi 35000/= badala ya shilingi 25000/= ambayo imepangwa na Sumatra.
Aidha ameendelea kufafanua kua CHAKUA  imeanzisha programu ya kuyafikisha mahakamani Mabasi yote yanayopata ajali na kusababisha madhara kwa  abiria,ili kusaidia abiria kulipwa fidia kwa urahisi na kwa muda mfupi.

Jumia Market kufanya punguzo la pei kwa asilimia 80 msimu wa sikukuu

Imebainishwa kuwa kufanyabiashara kwa njia ya mtandao hupunguza garama kubwa ya uendeshaji kibiashara kutokana na biashara za mitandao kuto hitaji eneo maalum la kufanyia biashara na kugarimu fedha kidogo na kuwafikia watu wengi zaidi.

Mkurugenzi Mtendaji wa ukanda wa Afrika Mashariki, kutoka kampuni ya uuzaji bidhaa kwanjia ya mtanda ya JUMIA – MARKET Bwana Justine Christianson ameiambia East Africa Radio katika mahojiano maalum kuusiana na biashara kwanjia ya mtandao, na kusema kuwa kunaurahisi mkubwa kuendesha biashara mitandaoni.
Huduma za mtandao zinamrahisishia mteja kununua na kupata bidhaa kwa wakati pamoja na kuepuka kutumia gharama za ziada kama usafiri kutokana na wateja kupelekewa bidhaa majumbani mwao” amesema
Christians, amesema katika nchi za Africa Mashariki Tanzania imeonekana kukuwa kwa shuguli za kimtandao huku nchi ya Kenya ikiongoza kwakufanya manunuzi mitandaoni ambapo aliwashauri vijana kutumia muda wao kubuni njia za kujipatia kipato bila kugarimu fedha mitandaoni.
Meneja Mkuu wa JUMIA MARKET nchini Tanzania Bwana Laurite Elmshauser amesema ili kuhakikisha watanzania wengi wanatumia mitandao kununua bidhaa, kampuni yao JUMIA imefanya punguzo la bei za bidhaa zake kwa asilimi 80 katika wiki yake ya maadhimisho ya Black Friday.
Meneja Masoko wa JUMIA MARKET Bi. Herrieth ngolwa amesema kampeni hiyo ijulikanayo kama Black Friday itakuwa ya siku 5 kuanzia Tarehe 21 Nov hadi 25 Nov ili kuwawezesha watanzania kununua bidhaa za msimu wa krismas kwa punguzo la pei kwa kutembelea mtandao wa JUMIA.





Kategori

Kategori